Zaburi 92

Wimbo wa kumsifu Mungu

(Zaburi. Wimbo wa siku ya Sabato)

1 Ni vema kukushukuru, ee Mwenyezi-Mungu,

kuliimbia sifa jina lako, ee Mungu Mkuu.

2 Ni vema kutangaza fadhili zako asubuhi,

na uaminifu wako nyakati za usiku,

3 kwa muziki wa zeze na kinubi,

kwa sauti tamu ya zeze.

4 Ee Mwenyezi-Mungu, matendo yako yanifurahisha;

nitashangilia kwa sababu ya mambo yote uliyotenda.

5 Matendo yako, ee Mwenyezi-Mungu, ni makuu mno!

Mawazo yako ni mazito mno!

6 Mtu mpumbavu hawezi kufahamu,

wala mjinga hajui jambo hili:

7 Kwamba waovu waweza kustawi kama nyasi,

watenda maovu wote waweza kufanikiwa,

lakini mwisho wao ni kuangamia milele,

8 bali wewe, ee Mwenyezi-Mungu, u mkuu milele.

9 Hao maadui zako, ee Mwenyezi-Mungu,

naam, hao maadui zako, hakika wataangamia;

wote watendao maovu, watatawanyika!

10 Wewe umenipa nguvu kama nyati;

umenimiminia mafuta ya kuburudisha.

11 Kwa macho nimeona maadui zangu wameshindwa;

nimesikia kilio chao watendao maovu.

12 Waadilifu hustawi kama mitende;

hukua kama mierezi ya Lebanoni!

13 Kama miti iliyopandwa nyumbani mwa Mwenyezi-Mungu,

hustawi katika nyua za Mungu wetu;

14 huendelea kuzaa matunda hata uzeeni;

daima wamejaa utomvu na wabichi;

15 wapate kutangaza kwamba Mwenyezi-Mungu ni mnyofu,

Mwamba wangu, kwake hamna upotovu.