Zaburi 93

Mungu mfalme

1 Mwenyezi-Mungu anatawala;

amejivika fahari kuu!

Mwenyezi-Mungu amevaa fahari na nguvu!

Ameuimarisha ulimwengu, nao hautatikisika kamwe.

2 Kiti chako cha enzi ni imara tangu kale;

wewe umekuwapo kabla ya nyakati zote.

3 Vilindi vimetoa sauti, ee Mwenyezi-Mungu;

naam, vimepaza sauti yake,

vilindi vyapaza tena mvumo wake.

4 Mwenyezi-Mungu ana enzi kuu juu mbinguni,

ana nguvu kuliko mlio wa bahari,

ana nguvu kuliko mawimbi ya maji.

5 Ee Mwenyezi-Mungu, maagizo yako ni thabiti;

nyumba yako ni takatifu milele na milele.