Zaburi 97

Mungu mtawala mkuu

1 Mwenyezi-Mungu anatawala!

Furahi, ee dunia!

Furahini enyi visiwa vingi!

2 Mawingu na giza nene vyamzunguka;

uadilifu na haki ni msingi wa utawala wake.

3 Moto watangulia mbele yake,

na kuwateketeza maadui zake pande zote.

4 Umeme wake wauangaza ulimwengu;

dunia yauona na kutetemeka.

5 Milima yayeyuka kama nta mbele ya Mwenyezi-Mungu;

naam, mbele ya Bwana wa dunia yote.

6 Mbingu zatangaza uadilifu wake;

na mataifa yote yauona utukufu wake.

7 Wote wanaoabudu sanamu wanaaibishwa,

naam, wote wanaojisifia miungu duni;

miungu yote husujudu mbele zake.

8 Watu wa Siyoni wanafurahi;

watu wa Yuda wanashangilia,

kwa sababu ya hukumu zako, ee Mungu.

9 Wewe Mwenyezi-Mungu ni mkuu juu ya dunia yote;

wewe watukuka juu ya miungu yote.

10 Mwenyezi-Mungu huwapenda wanaochukia uovu,

huyalinda maisha ya watu wake;

huwaokoa makuchani mwa waovu.

11 Mwanga humwangazia mtu mwadilifu,

na furaha kwa watu wanyofu wa moyo.

12 Furahini kwa sababu ya Mwenyezi-Mungu enyi waadilifu;

mshukuruni kwa ajili ya jina lake takatifu.