Zaburi 98

Mungu mtawala wa dunia yote

1 Mwimbieni Mwenyezi-Mungu wimbo mpya,

kwa maana ametenda mambo ya ajabu!

Mkono wake hodari, mkono wake mtakatifu umempatia ushindi.

2 Mwenyezi-Mungu ameonesha ushindi wake;

ameyadhihirishia mataifa uwezo wake wa kuokoa.

3 Amekumbuka fadhili na uaminifu wake kwa Waisraeli.

Pande zote za dunia zimeuona ushindi wa Mungu wetu.

4 Dunia yote imshangilie Mwenyezi-Mungu;

imsifu kwa nyimbo na vigelegele.

5 Msifuni Mwenyezi-Mungu kwa shangwe,

msifuni kwa sauti tamu za zeze.

6 Mpigieni vigelegele Mwenyezi-Mungu mfalme wetu,

mshangilieni kwa tarumbeta na sauti ya baragumu.

7 Bahari na ivume na vyote vilivyomo;

dunia na wote waishio ndani yake.

8 Enyi mito pigeni makofi;

enyi vilima imbeni pamoja kwa shangwe.

9 Shangilieni mbele ya Mwenyezi-Mungu,

maana anakuja kutawala dunia.

Atauhukumu ulimwengu kwa haki,

atawatawala watu kwa uadilifu.