Isaya 12

Wimbo wa shukrani

1 Siku hiyo mtasema:

“Nakushukuru, ee Mwenyezi-Mungu,

maana ingawa ulinikasirikia,

hasira yako imetulia,

nawe umenifariji.

2 Mungu ndiye mwenye kuniokoa,

nitamtegemea yeye, wala sitaogopa;

Mwenyezi-Mungu hunijalia nguvu;

yeye mwenyewe ndiye aniokoaye.”

3 Mtachota maji kwa furaha

kutoka visima vya wokovu.

4 Siku hiyo mtasema:

“Mshukuruni Mwenyezi-Mungu

mwombeni kwa jina lake.

Yajulisheni mataifa matendo yake,

tangazeni kuwa jina lake limetukuka.

5 Mwimbieni Mwenyezi-Mungu sifa

kwa kuwa ametenda mambo makuu;

haya na yajulikane duniani kote.

6 Pazeni sauti na kuimba kwa furaha,

enyi wakazi wa Siyoni,

maana aliye mkuu miongoni mwenu

ndiye Mungu, Mtakatifu wa Israeli.”