Ulimwengu wote umsifu Mungu
1 Msifuni Mwenyezi-Mungu!
Msifuni Mwenyezi-Mungu kutoka mbinguni,
msifuni kutoka huko juu mbinguni.
2 Msifuni, enyi malaika wake wote,
msifuni, enyi majeshi yake yote.
3 Msifuni, enyi jua na mwezi,
msifuni, enyi nyota zote zingaazo.
4 Msifuni, enyi mbingu za juu,
na maji yaliyo juu ya mbingu.
5 Vyote vilisifu jina la Mwenyezi-Mungu,
maana yeye aliamuru, na vyote vikawa.
6 Yeye aliviweka mahali pao daima,
kwa amri ambayo haiwezi kubatilishwa.
7 Msifuni Mwenyezi-Mungu kutoka duniani;
enyi majoka ya baharini na vilindini, msifuni.
8 Msifuni enyi moto, mvua ya mawe na theluji,
upepo wa tufani unaotimiza amri yake!
9 Msifuni enyi milima na vilima,
miti ya matunda na misitu!
10 Msifuni enyi wanyama wa porini na wafugwao,
viumbe vitambaavyo na ndege wote!
11 Msifuni enyi wafalme na mataifa yote;
viongozi na watawala wote duniani!
12 Msifuni enyi wavulana na wasichana;
wazee wote na watoto pia!
13 Nyote lisifuni jina la Mwenyezi-Mungu,
maana jina lake peke yake latukuka;
utukufu wake wapita dunia na mbingu.
14 Amewapa watu wake nguvu;
heshima kwa watu wote waaminifu,
watu wa Israeli wapenzi wake.
Msifuni Mwenyezi-Mungu!