Zaburi 142

Dua ya mtu aliyeachwa mpweke

(Utenzi wa Daudi alipokuwa pangoni. Sala)

1 Namlilia Mwenyezi-Mungu kwa sauti,

namsihi Mwenyezi-Mungu kwa sauti yangu.

2 Namwekea malalamiko yangu,

namweleza taabu zangu.

3 Ninapokaribia kukata tamaa kabisa,

yeye yupo, anajua mwenendo wangu.

Maadui wamenitegea mitego njiani mwangu.

4 Nikiangalia upande wa kulia na kungojea,

naona hakuna mtu wa kunisaidia;

sina tena mahali pa kukimbilia,

hakuna mtu anayenijali.

5 Nakulilia wewe, ee Mwenyezi-Mungu!

Wewe ni kimbilio langu la usalama;

wewe ni riziki yangu kuu katika nchi ya walio hai.

6 Usikilize kilio changu, maana nimekuwa hoi;

uniokoe na watesi wangu, maana wamenizidi nguvu.

7 Unitoe humu kifungoni,

ili nipate kukushukuru.

Watu waadilifu watajiunga nami

kwa sababu umenitendea mema mengi.