Zaburi 138

Sala ya shukrani

1 Nakushukuru, ee Mwenyezi-Mungu, kwa moyo wangu wote,

naimba sifa zako mbele ya miungu.

2 Ninasujudu kuelekea hekalu lako takatifu;

nalisifu jina lako,

kwa sababu ya fadhili zako na uaminifu wako;

kwa sababu umeweka jina lako na neno lako

juu ya kila kitu.

3 Nilipokulilia, wewe ulinijibu;

umeniongezea nguvu zangu.

4 Wafalme wote duniani watakusifu, ee Mwenyezi-Mungu,

kwa sababu wameyasikia maneno yako.

5 Wataimba sifa za matendo yako, ee Mwenyezi-Mungu,

kwa maana utukufu wako ni mkuu.

6 Ingawa wewe ee Mwenyezi-Mungu, uko juu ya wote,

unawaangalia kwa wema walio wanyonge;

nao wenye kiburi huwaona kutoka mbali.

7 Hata nikikumbana na taabu, wewe wanilinda;

waunyosha mkono wako dhidi ya hasira ya maadui zangu wakali;

kwa nguvu yako kuu wanisalimisha.

8 Ee Mwenyezi-Mungu, utatimiza yote uliyoniahidi.

Fadhili zako, ee Mwenyezi-Mungu, zadumu milele.

Usisahau kazi ya mkono wako mwenyewe.