Zaburi 137

Ombolezo ugenini

1 Kando ya mito ya Babuloni, tulikaa,

tukawa tunalia tulipokumbuka Siyoni.

2 Katika miti ya nchi ile,

tulitundika zeze zetu.

3 Waliotuteka walitutaka tuwaimbie;

watesi wetu walitutaka tuwafurahishe:

“Tuimbieni mojawapo ya nyimbo za Siyoni!”

4 Twawezaje kuimba wimbo wa Mwenyezi-Mungu

katika nchi ya kigeni?

5 Ee Yerusalemu, kama nikikusahau,

mkono wangu wa kulia na ukauke!

6 Ulimi wangu na uwe mzito,

kama nisipokukumbuka wewe, ee Yerusalemu;

naam, nisipokuthamini kuliko furaha yangu kubwa!

7 Ee Mwenyezi-Mungu, usisahau waliyotenda Waedomu,

siku ile Yerusalemu ilipotekwa;

kumbuka waliyosema:

“Bomoeni mji wa Yerusalemu!

Ngoeni hata na misingi yake!”

8 Ee Babuloni, utaangamizwa!

Heri yule atakayekulipiza mabaya uliyotutenda!

9 Heri yule atakayewatwaa watoto wako

na kuwapondaponda mwambani!