Sifa ya nyumba ya Mungu
(Wimbo wa Kwenda Juu)
1 Ee Mwenyezi-Mungu, mkumbuke Daudi,
kumbuka taabu zote alizopata.
2 Ukumbuke ahadi aliyokupa, ee Mwenyezi-Mungu,
kiapo alichokuapia, ewe Mwenye Nguvu wa Yakobo:
3 “Sitaingia ndani ya nyumba yangu,
wala kulala kitandani mwangu;
4 sitakubali kulala usingizi,
wala kusinzia;
5 mpaka nikupatie wewe Mwenyezi-Mungu mahali pa kukaa,
makao yako, ewe Mwenye Nguvu wa Yakobo!”
6 Huko Efratha tulisikia habari za sanduku la agano,
tukalikuta katika mashamba ya Yearimu.
7 “Haya! Twende nyumbani kwa Mungu,
tuabudu mbele ya kiti chake cha enzi!”
8 Inuka ee Mwenyezi-Mungu, nenda kwenye maskani yako;
inuka pamoja na sanduku la agano la uwezo wako!
9 Makuhani wako wawe waadilifu daima;
na waaminifu wako wapige vigelegele vya furaha!
10 Kwa ajili ya Daudi, mtumishi wako,
usimkatae huyo mfalme uliyemweka wakfu.
11 Mwenyezi-Mungu alimwapia Daudi kiapo thabiti,
kiapo ambacho hatakibatilisha:
“Nitamtawaza mmoja wa wazawa wako mwenyewe,
kuwa mfalme baada yako.
12 Watoto wako wakishika agano langu,
na kuzingatia mafundisho nitakayowapa,
watoto wao pia watakuwa wafalme kama wewe.”
13 Mwenyezi-Mungu ameuchagua mji wa Siyoni,
ametaka uwe makao yake:
14 “Hapa ndipo nitakapokaa milele,
ndipo maskani yangu maana nimepachagua.
15 Nitaubariki sana mji wa Siyoni kwa mahitaji yake;
nitawashibisha chakula maskini wake.
16 Nitawafanikisha makuhani wake kwa wokovu;
waaminifu wake watapiga vigelegele vya furaha.
17 Humo nitamchipusha mfalme shujaa wa ukoo wa Daudi:
Kama taa iwakayo nitamtegemeza mfalme niliyemteua.
18 Maadui zake nitawavika aibu;
lakini yeye nitamvika fahari ya kifalme.”