Zaburi 128

Tuzo kwa jamaa imchayo Mungu

(Wimbo wa Kwenda Juu)

1 Heri wote wamchao Mwenyezi-Mungu,

wanaoishi kufuatana na amri zake.

2 Utapata matunda ya jasho lako,

utafurahi na kupata fanaka.

3 Mkeo atakuwa kama mzabibu wa matunda mengi nyumbani mwako;

watoto wako kama chipukizi za mzeituni kuzunguka meza yako.

4 Naam, ndivyo atakavyobarikiwa

mtu amchaye Mwenyezi-Mungu.

5 Mwenyezi-Mungu akubariki kutoka Siyoni!

Uione fanaka ya Yerusalemu, siku zote za maisha yako.

6 Uishi na hata uwaone wajukuu zako!

Amani iwe na Israeli!