Kuomba nguvu mpya
(Wimbo wa Kwenda Juu)
1 Mwenyezi-Mungu alipoturekebisha na kuturudisha Siyoni,
tulikuwa kama watu wanaoota ndoto!
2 Hapo tuliangua kicheko;
tulishangilia kwa furaha.
Nao watu wa mataifa mengine walisema:
“Mwenyezi-Mungu amewatendea mambo makubwa!”
3 Kweli Mwenyezi-Mungu alitutendea mambo makubwa,
tulifurahi kwelikweli!
4 Ee Mwenyezi-Mungu, urekebishe tena hali yetu,
kama mvua inavyotiririsha maji katika mabonde makavu.
5 Wanaopanda kwa machozi,
watavuna kwa shangwe.
6 Wanaokwenda kupanda mbegu wakilia,
watarudi kwa furaha wakichukua mavuno.