Zaburi 118

Sala ya shukrani

1 Mshukuruni Mwenyezi-Mungu, kwa kuwa ni mwema,

kwa maana fadhili zake zadumu milele.

2 Watu wa Israeli na waseme:

“Fadhili zake zadumu milele.”

3 Wazawa wa Aroni na waseme:

“Fadhili zake zadumu milele.”

4 Wote wamchao Mwenyezi-Mungu na waseme:

“Fadhili zake zadumu milele.”

5 Katika taabu yangu nilimwomba Mwenyezi-Mungu,

naye akanisikia na kuniweka huru.

6 Mwenyezi-Mungu yuko nami, siogopi kitu;

binadamu ataweza kunifanya nini?

7 Mwenyezi-Mungu yuko nami, kunisaidia;

nami nitawaona maadui zangu wameshindwa.

8 Afadhali kukimbilia usalama kwa Mwenyezi-Mungu,

kuliko kumtumainia mwanadamu.

9 Afadhali kukimbilia usalama kwa Mwenyezi-Mungu,

kuliko kuwatumainia viongozi wa dunia.

10 Mataifa yote yalinizingira,

lakini kwa jina la Mwenyezi-Mungu nikayaangamiza!

11 Yalinizunguka kila upande,

lakini kwa jina la Mwenyezi-Mungu, nikayaangamiza!

12 Yalinizunguka, mengi kama nyuki,

lakini yakateketea kama kichaka motoni;

kwa jina la Mwenyezi-Mungu niliyaangamiza!

13 Nilishambuliwa mno karibu nishindwe,

lakini Mwenyezi-Mungu alinisaidia.

14 Mwenyezi-Mungu ni nguvu yangu kuu;

yeye mwenyewe ndiye wokovu wangu.

15 Sauti za furaha ya ushindi zasikika hemani mwao waadilifu:

“Mkono wa Mwenyezi-Mungu umetenda mambo makuu!

16 Mkono wa nguvu wa Mwenyezi-Mungu umeleta ushindi!

Mkono wa Mwenyezi-Mungu umetenda mambo makuu!”

17 Sitakufa, bali nitaishi,

na kusimulia matendo ya Mwenyezi-Mungu.

18 Mwenyezi-Mungu ameniadhibu sana,

lakini hakuniacha nife.

19 Nifungulie milango ya watu waadilifu,

niingie na kumshukuru Mwenyezi-Mungu!

20 Huu ndio mlango wa Mwenyezi-Mungu,

watu waadilifu watapitia humo.

21 Nakushukuru, ee Mungu kwa kunijibu;

kwa sababu wewe ni wokovu wangu.

22 Jiwe walilokataa waashi,

limekuwa jiwe kuu la msingi.

23 Hiyo ni kazi yake Mwenyezi-Mungu

nayo ni ya ajabu sana kwetu.

24 Hii ndiyo siku aliyoifanya Mwenyezi-Mungu;

tushangilie na kufurahi.

25 Tafadhali utuokoe, ee Mwenyezi-Mungu!

Tafadhali utufanikishe, ee Mwenyezi-Mungu!

26 Abarikiwe huyo ajaye kwa jina la Mwenyezi-Mungu!

Twawabariki kutoka nyumbani mwa Mwenyezi-Mungu

27 Mwenyezi-Mungu ni Mungu;

yeye ametujalia mwanga wake

Shikeni matawi ya sherehe,

mkiandamana mpaka madhabahuni.

28 Wewe ni Mungu wangu, nami ninakushukuru;

ninakutukuza, ee Mungu wangu.

29 Mshukuruni Mwenyezi-Mungu kwa kuwa ni mwema,

kwa maana fadhili zake zadumu milele.