Shukrani kwa kuokolewa kifoni
1 Nampenda Mwenyezi-Mungu,
kwa maana anisikia,
maana amesikia kilio cha ombi langu.
2 Yeye amenitegea sikio,
hivyo nitamwomba muda wote niishio.
3 Hatari ya kifo ilinizunguka,
vitisho vya kaburi vilinivamia;
nilijawa na mahangaiko na majonzi.
4 Kisha nikamlilia Mwenyezi-Mungu:
“Ee Mwenyezi-Mungu, tafadhali unisalimishe!”
5 Mwenyezi-Mungu amejaa wema na uaminifu;
Mungu wetu ni mwenye huruma.
6 Mwenyezi-Mungu huwalinda wanyofu;
nilipokuwa nimekandamizwa aliniokoa.
7 Uwe na utulivu mkuu, ee nafsi yangu,
maana Mwenyezi-Mungu amenitendea mema.
8 Ameniokoa kifoni na kufuta machozi yangu;
akanilinda nisije nikaanguka.
9 Nitatembea mbele yake Mwenyezi-Mungu,
katika nchi ya watu walio hai.
10 Nilikuwa na imani hata niliposema:
“Mimi nimetaabika mno.”
11 Hata nilisema kwa hofu yangu:
“Binadamu wote hawaaminiki!”
12 Nimrudishie nini Mwenyezi-Mungu,
kwa ukarimu wote alionitendea?
13 Nitamtolea tambiko ya divai kwa kunikomboa,
nitaomba kwa jina lake Mwenyezi-Mungu.
14 Nitamtimizia Mwenyezi-Mungu nadhiri zangu,
mbele ya watu wake wote.
15 Kifo cha waaminifu wake Mwenyezi-Mungu
si jambo dogo mbele yake.
16 Ee Mwenyezi-Mungu, mimi ni mtumishi wako;
ni mtumishi wako, mtoto wa mjakazi wako;
umenifungulia vifungo vyangu.
17 Nitakutolea tambiko za shukrani,
na kukupa heshima zangu.
18 Nitakutimizia ahadi zangu, ee Mwenyezi-Mungu
mbele ya watu wako wote,
19 waliokusanyika hekaluni mwako,
katikati ya Yerusalemu.
Msifuni Mwenyezi-Mungu!