Furaha ya mtu mwema
1 Msifuni Mwenyezi-Mungu!
Heri mtu anayemcha Mwenyezi-Mungu,
anayefurahia sana kutii amri zake.
2 Wazawa wake watakuwa wenye nguvu nchini;
watoto wa wanyofu watapata baraka.
3 Nyumbani kwake kutakuwa na mali nyingi;
uadilifu wake wadumu milele.
4 Mtu mwema huangaziwa mwanga gizani;
mtu mwenye huruma, mpole na mwadilifu.
5 Mtu mkarimu akopeshaye bila faida, hufanikiwa;
mtu afanyaye shughuli zake kwa kutumia haki.
6 Mwadilifu hatashindwa kamwe,
huyo atakumbukwa milele.
7 Hana haja ya kuogopa akipata habari mbaya;
ana moyo thabiti na humtegemea Mwenyezi-Mungu.
8 Yuko imara moyoni, wala hataogopa;
naye atawaona maadui zake wanashindwa.
9 Hutoa kwa ukarimu, huwapa maskini;
uadilifu wake wadumu milele.
Nguvu yake inatukuzwa kwa heshima.
10 Watu waovu huona hayo na kuudhika;
husaga meno kwa chuki na kutoweka,
matazamio ya mtu mbaya huishia patupu.