Zaburi 95

Utenzi wa kumsifu Mungu

1 Njoni tumwimbie Mwenyezi-Mungu,

tumshangilie mwamba wa wokovu wetu!

2 Twende mbele zake na shukrani;

tumshangilie kwa nyimbo za sifa.

3 Maana Mwenyezi-Mungu, ni Mungu mkuu;

yeye ni Mfalme mkuu juu ya miungu yote.

4 Vilindi vyote vya dunia vimo mikononi mwake,

vilele vya milima ni vyake.

5 Bahari ni yake, ndiye aliyeifanya;

kwa mikono yake aliiumba nchi kavu.

6 Njoni tusujudu na kumwabudu;

tumpigie magoti Mwenyezi-Mungu, Muumba wetu!

7 Maana yeye ni Mungu wetu,

nasi ni watu wa kundi lake,

ni kondoo wake anaowachunga.

Laiti leo mngesikiliza sauti yake:

8 “Msiwe wakaidi kama kule Meriba,

kama walivyokuwa kule Masa jangwani,

9 wazee wenu waliponijaribu na kunipima,

ingawa walikuwa wameona mambo niliyowatendea.

10 Kwa miaka arubaini nilichukizwa nao,

nikasema: ‘Kweli, hawa ni watu waliopotoka!

Hawajali kabisa njia zangu!’

11 Basi, nilikasirika, nikaapa:

‘Hawataingia mahali pangu pa pumziko!’”