Zaburi 86

Kuomba msaada

(Sala ya Daudi)

1 Unitegee sikio, ee Mwenyezi-Mungu, unijibu,

maana mimi ni fukara na mnyonge.

2 Uyahifadhi maisha yangu maana mimi ni mchaji wako;

uniokoe mimi mtumishi wako ninayekutegemea.

3 Wewe ni Mungu wangu;

basi, unionee huruma,

maana nakulilia mchana kutwa.

4 Uifurahishe roho yangu mimi mtumishi wako,

maana sala zangu nazielekeza kwako ee Bwana.

5 Wewe, ee Bwana, u mwema na mwenye kusamehe;

mwingi wa fadhili kwa wote wakuombao.

6 Ee Mwenyezi-Mungu, uitegee sikio sala yangu;

ukisikie kilio cha ombi langu.

7 Siku za taabu nakuita,

maana wewe waniitikia.

8 Ee Bwana, hakuna Mungu aliye kama wewe;

hakuna awezaye kufanya unayofanya wewe.

9 Mataifa yote uliyoyaumba, yatakuja kukuabudu, ee Bwana;

yatatangaza ukuu wa jina lako.

10 Wewe ndiwe mkuu, wafanya maajabu;

wewe peke yako ndiwe Mungu.

11 Unifundishe njia yako, ee Mwenyezi-Mungu,

nipate kuwa mwaminifu kwako;

uongoze moyo wangu nikuheshimu.

12 Ee Bwana, Mungu wangu, nitakusifu kwa moyo wote;

nitatangaza ukuu wa jina lako milele.

13 Fadhili zako kwangu ni nyingi mno!

Umeniokoa kutoka chini kuzimu.

14 Ee Mungu, watu wenye kiburi wamenikabili;

kundi la watu wakatili wanataka kuniua,

wala hawakujali wewe hata kidogo.

15 Lakini wewe Bwana, ni Mungu wa rehema na huruma;

wewe ni mvumilivu, mwingi wa fadhili na uaminifu.

16 Unigeukie, unihurumie;

unijalie nguvu yako mimi mtumishi wako,

umwokoe mtoto wa mjakazi wako.

17 Unioneshe ishara ya wema wako, ee Mwenyezi-Mungu,

ili wale wanaonichukia waaibike,

waonapo umenisaidia na kunifariji.