Zaburi 85

Kuliombea fanaka taifa

(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Wakorahi)

1 Ee Mwenyezi-Mungu,

umeifadhili nchi yako;

umemjalia Yakobo bahati nzuri tena.

2 Umewasamehe watu wako kosa lao;

umezifuta dhambi zao zote.

3 Umeizuia ghadhabu yako yote;

umeiacha hasira yako kali.

4 Uturekebishe tena, ee Mungu mwokozi wetu;

uiondoe chuki uliyo nayo juu yetu.

5 Je, utatukasirikia hata milele?

Je, utadumisha ghadhabu yako kwa vizazi vyote?

6 Je, hutatujalia tena maisha mapya,

ili watu wako wafurahi kwa sababu yako?

7 Utuoneshe, fadhili zako, ee Mwenyezi-Mungu,

utujalie wokovu wako.

8 Hebu nisikie anachosema Mwenyezi-Mungu;

maana anaahidi kuwapa watu wake amani,

watu wake mwenyewe wasiporudia upuuzi wao

9 Hakika yu tayari kuwaokoa wanaomheshimu,

na utukufu wake utadumu nchini mwetu.

10 Fadhili zake na uaminifu vitakutana;

uadilifu na amani vitaungana.

11 Uaminifu utachipuka katika nchi;

uadilifu utashuka toka mbinguni.

12 Naam, Mwenyezi-Mungu atatuletea fanaka,

na nchi yetu itatoa mazao yake mengi.

13 Uadilifu utamtangulia Mungu

na kumtayarishia njia yake.