Zaburi 82

Mungu mtawala mkuu

(Zaburi ya Asafu)

1 Mungu anasimamia baraza lake;

anatoa hukumu katika kusanyiko la miungu:

2 “Mpaka lini mtaendelea kuhukumu bila haki

na kuwapendelea watu waovu?

3 Wapeni wanyonge na yatima haki zao;

tekelezeni haki za wanaoonewa na fukara.

4 Waokoeni wanyonge na maskini,

waokoeni makuchani mwa wadhalimu.

5 “Lakini nyinyi hamjui wala hamfahamu!

Nyinyi mnatembea katika giza la upotovu!

Misingi yote ya haki duniani imetikiswa!

6 Mimi nilisema kuwa nyinyi ni miungu;

kwamba nyote ni watoto wa Mungu Mkuu!

7 Hata hivyo, mtakufa kama watu wote;

mtaanguka kama mkuu yeyote.”

8 Inuka ee Mungu, uuhukumu ulimwengu;

maana mataifa yote ni mali yako.