Zaburi 81

Wimbo wa sikukuu

(Kwa Mwimbishaji: Mtindo wa Gitithi. Zaburi ya Asafu)

1 Mwimbieni kwa sauti Mungu, nguvu yetu,

mshangilieni Mungu wa Yakobo;

2 vumisheni wimbo wa shangwe, pigeni ngoma,

chezeni zeze na kinubi cha sauti nzuri.

3 Pigeni tarumbeta kutangaza mwezi mwandamo,

na pia mwezi mpevu, wakati wa sikukuu yetu.

4 Hiyo ndiyo kanuni katika Israeli;

hilo ndilo agizo la Mungu wa Yakobo.

5 Aliwapa watu wa Israeli agizo hilo,

alipoishambulia nchi ya Misri.

Nasikia sauti nisiyoitambua ikisema:

6 “Mimi nilikutua mizigo yako mabegani,

nilikuondolea matofali uliyochukua mikononi.

7 Ukiwa shidani uliniita, nami nikakuokoa.

Nilikujibu nikiwa mafichoni katika ngurumo.

Nilikujaribu kwenye maji ya Meriba.

8 Enyi watu wangu, sikieni onyo langu.

Laiti ungenisikiliza, ee Israeli!

9 Asiwepo kwako mungu wa kigeni;

usiabudu kamwe mungu mwingine.

10 Mimi ndimi Mwenyezi-Mungu, Mungu wako,

niliyekutoa katika nchi ya Misri.

Fumbua kinywa chako, nami nitakulisha.

11 “Lakini watu wangu hawakunisikiliza;

Israeli hakunitaka kabisa.

12 Hivyo, nikawaacha wabaki na ukaidi wao;

wafuate mashauri yao wenyewe.

13 Laiti watu wangu wangenisikiliza!

Laiti Israeli angefuata njia yangu!

14 Ningewashinda maadui zao haraka;

ningenyosha mkono dhidi ya wadhalimu wao.

15 Wanichukiao wangenipigia magoti kwa hofu,

na adhabu yao ingekuwa ya milele.

16 Lakini wewe ningekulisha kwa ngano bora,

ningekushibisha kwa asali ya mwambani.”