Zaburi 80

Maombi kwa ajili ya taifa

(Kwa Mwimbishaji: Mtindo wa Yungiyungi. Zaburi ya Asafu)

1 Utege sikio, ewe Mchungaji wa Israeli,

uwaongozaye wazawa wa Yosefu kama kondoo.

Ewe ukaaye juu ya viumbe vyenye mabawa,uangaze,

2 mbele ya Efraimu, Benyamini na Manase.

Uoneshe nguvu yako, uje kutuokoa!

3 Uturekebishe, ee Mungu;

utuangalie kwa wema, nasi tutaokoka.

4 Ee Mwenyezi-Mungu, Mungu wa majeshi,

hata lini utazikasirikia sala za watu wako?

5 Umefanya huzuni iwe chakula chetu;

umetunywesha machozi kwa wingi.

6 Umetufanya tuwe dharau kwa jirani zetu;

maadui zetu wanatudhihaki.

7 Ee Mungu wa majeshi, uturekebishe,

utuangalie kwa wema, nasi tutaokoka.

8 Ulileta mzabibu kutoka Misri;

ukawafukuza watu wa mataifa mengine,

na kuupanda katika nchi yao.

9 Uliupalilia upate kukua,

nao ukatoa mizizi na kuenea kote nchini.

10 Uliifunika milima kwa kivuli chake,

na matawi yake yakawa kama mierezi mikubwa.

11 Matawi yake yalienea mpaka baharini;

machipukizi yake mpaka kando ya mto Eufrate.

12 Mbona ulibomoa kuta zilizouzunguka?

Sasa kila apitaye anachuma zabibu zake;

13 nguruwe mwitu wanauharibu,

na wanyama wa porini wanautafuna!

14 Utugeukie tena ee Mungu wa majeshi.

Uangalie toka mbinguni, uone;

ukautunze mzabibu huo.

15 Uulinde mche ulioupanda kwa mkono wako;

hilo chipukizi uliloimarisha wewe mwenyewe.

16 Watu walioukata na kuuteketeza,

uwatazame kwa ukali, waangamie.

17 Mkono wako umkinge huyo uliyemfadhili;

huyo uliyemteua kwa ajili yako.

18 Hatutakuacha na kukuasi tena;

utujalie uhai, nasi tutakusifu.

19 Ee Mwenyezi-Mungu wa majeshi uturekebishe;

utuangalie kwa wema, nasi tutaokoka.