Zaburi 76

Mungu mshindi

(Kwa Mwimbishaji: Na ala za nyuzi za muziki. Zaburi ya Asafu. Wimbo)

1 Mungu anajulikana katika Yuda;

jina lake ni kuu katika Israeli.

2 Makao yake yamo huko Salemu;

maskani yake huko Siyoni.

3 Huko alivunja mishale ya adui;

alivunja ngao, panga na silaha za vita.

4 Wewe, ee Mungu, watukuka mno;

umejaa fahari kuliko milima ya milele.

5 Wenye nguvu walipokonywa nyara zao,

sasa wamelala usingizi wa kifo,

mashujaa wa vita hawakuweza kutumia mikono yao.

6 Ulipowakemea, ee Mungu wa Yakobo,

farasi na wapandafarasi walikufa ganzi.

7 Wewe, ee Mungu, ni wa kutisha mno!

Nani awezaye kustahimili mbele yako ukikasirika?

8 Ulijulisha hukumu yako toka mbinguni;

dunia iliogopa na kunyamaza;

9 wakati ulipoinuka kutekeleza hukumu,

kuwaokoa wote wanaodhulumiwa duniani.

10 Ghadhabu ya watu husababisha tu sifa kwako;

na waliookoka vitani watafanya sikukuu zako.

11 Mtimizieni Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu ahadi zenu;

enyi mlio karibu mpeni zawadi Mungu wa kutisha.

12 Yeye huzitoa roho za wakuu;

huwatisha wafalme wa dunia.