Zaburi 52

Hukumu ya Mungu

(Kwa Mwimbishaji. Utenzi wa Daudi baada ya Doegi, Mwedomu, kumwendea Shauli na kumjulisha kuwa Daudi amekwenda nyumbani kwa Abimeleki)

1 Mbona, ewe jitu, wajivunia ubaya wako

dhidi ya wenye kumcha Mungu?

2 Kila wakati unawaza maangamizi;

ulimi wako ni kama wembe mkali!

Unafikiria tu kutenda mabaya.

3 Wewe wapenda uovu kuliko wema,

wapenda uongo kuliko ukweli.

4 Ewe mdanganyifu mkuu,

wapenda mambo ya kuangamiza wengine.

5 Kwa hivyo Mungu atakuangamiza milele,

atakunyakua na kukuondoa nyumbani mwako;

atakungoa katika nchi ya walio hai.

6 Waadilifu wataona hayo na kuogopa,

kisha watakucheka na kusema:

7 “Tazameni yaliyompata mtu huyu!

Yeye hakutaka Mungu awe kimbilio lake;

bali alitegemea wingi wa mali yake,

na kutafuta humo usalama wake!”

8 Lakini mimi ni kama mzeituni mbichi,

unaostawi katika nyumba ya Mungu.

Nazitegemea fadhili zake milele na milele.

9 Ee Mungu, nitakushukuru daima,

kwa ajili ya mambo uliyofanya.

Nitatangaza kwamba wewe ni mwema,

mbele ya watu wako waaminifu.