Zaburi 43

Sala ya mkimbizi yaendelea

(Zaburi ya 42 yaendelea)

1 Onesha kuwa sina hatia ee Mungu;

utetee kisa changu dhidi ya watu wabaya;

uniokoe na watu waongo na waovu.

2 Nakimbilia usalama kwako ee Mungu;

kwa nini umenitupilia mbali?

Yanini niende huko na huko nikiomboleza

kwa kudhulumiwa na adui yangu?

3 Upeleke mwanga na ukweli wako viniongoze,

vinipeleke kwenye mlima wako mtakatifu,

kwenye makao yako.

4 Hapo, ee Mungu, nitakwenda madhabahuni pako;

nitakuja kwako, ee Mungu, furaha yangu kuu.

Nitakusifu kwa zeze, ee Mungu, Mungu wangu.

5 Mbona ninahuzunika hivyo moyoni?

Kwa nini nahangaika hivyo ndani mwangu?

Nitamtumainia Mungu,

nitamsifu tena

yeye aliye msaada wangu na Mungu wangu.