Zaburi 41

Sala ya mgonjwa

(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Daudi)

1 Heri mtu anayewajali maskini;

Mwenyezi-Mungu atamwokoa wakati wa shida.

2 Mwenyezi-Mungu atamlinda na kumweka hai,

naye atafanikiwa katika nchi;

Mungu hatamwacha makuchani mwa maadui zake.

3 Mwenyezi-Mungu atamsaidia awapo mgonjwa,

atamponya maradhi yake yote.

4 Nami nilisema: “Unifadhili, ee Mwenyezi-Mungu,

unihurumie maana nimekukosea wewe.”

5 Madui zangu husema vibaya juu yangu:

“Atakufa lini na jina lake litoweke!”

6 Wanitembeleapo husema maneno matupu;

wanakusanya mabaya juu yangu,

na wafikapo nje huwatangazia wengine.

7 Wote wanichukiao hunongonezana juu yangu;

wananiwazia mabaya ya kunidhuru.

8 Husema: “Maradhi haya yatamuua;

hatatoka tena kitandani mwake!”

9 Hata rafiki yangu wa moyoni niliyemwamini,

rafiki ambaye alishiriki chakula changu,

amegeuka kunishambulia!

10 Ee Mwenyezi-Mungu, unionee huruma!

Unipe nafuu, nami nitawalipiza.

11 Hivyo nitajua kwamba unapendezwa nami,

maadui zangu wasipopata fahari juu yangu.

12 Wewe umenitegemeza kwani natenda mema;

waniweka mbele yako milele.

13 Asifiwe Mwenyezi-Mungu, Mungu wa Israeli,

tangu milele na hata milele!

Amina! Amina!