Zaburi 32

Maondoleo ya dhambi

(Zaburi ya Daudi. Funzo)

1 Heri yake mtu aliyesamehewa kosa lake,

mtu ambaye dhambi yake imeondolewa kabisa.

2 Heri mtu ambaye Mwenyezi-Mungu hamwekei hatia,

mtu ambaye hana hila moyoni mwake.

3 Wakati nilipokuwa sijakiri dhambi yangu,

nilikuwa nimedhoofika kwa kulia mchana kutwa.

4 Mchana na usiku mkono wako ulinilemea;

nikafyonzwa nguvu zangu,

kama maji wakati wa kiangazi.

5 Kisha nilikiri makosa yangu kwako;

wala sikuuficha uovu wangu.

Nilisema ninakuungamia makosa yangu ee Mwenyezi-Mungu,

ndipo nawe ukanisamehe dhambi zangu zote.

6 Kwa hiyo, kila mwaminifu na akuletee maombi;

jeshi likaribiapo au mafuriko,

hayo hayatamfikia yeye.

7 Wewe ndiwe kinga yangu;

wewe wanilinda katika taabu.

Umenijalia shangwe za kukombolewa.

8 Mungu asema: “Nitakufunza

na kukuonesha njia unayopaswa kufuata.

Nitakushauri kwa uangalifu mkubwa.

9 Usiwe mpumbavu kama farasi au nyumbu,

ambao lazima wafungwe lijamu na hatamu,

la sivyo hawatakukaribia.”

10 Watu waovu watapata mateso mengi,

bali wanaomtumainia Mwenyezi-Mungu wazungukwa na fadhili zake.

11 Furahini na kushangilia kwa sababu ya Mwenyezi-Mungu enyi waadilifu;

pigeni vigelegele vya shangwe enyi wanyofu wa moyo.