Zaburi 29

Sauti ya Mungu katika dhoruba

(Zaburi ya Daudi)

1 Mpeni Mwenyezi-Mungu heshima enyi viumbe vya mbinguni,

semeni Mwenyezi-Mungu ni mtukufu na mwenye nguvu.

2 Semeni jina la Mwenyezi-Mungu ni tukufu.

Mwabuduni katika mahali pake patakatifu.

3 Sauti ya Mwenyezi-Mungu yasikika juu ya maji;

Mungu mtukufu angurumisha radi,

sauti ya Mwenyezi-Mungu yasikika juu ya bahari!

4 Sauti ya Mwenyezi-Mungu ina nguvu,

sauti ya Mwenyezi-Mungu imejaa fahari.

5 Sauti ya Mwenyezi-Mungu huvunja mierezi;

Mwenyezi-Mungu avunja mierezi ya Lebanoni.

6 Huirusha milima ya Lebanoni kama ndama,

milima ya Sirionikama mwananyati.

7 Sauti ya Mwenyezi-Mungu hutoa miali ya moto.

8 Sauti ya Mwenyezi-Mungu hutetemesha jangwa,

Mwenyezi-Mungu hutetemesha jangwa la Kadeshi.

9 Sauti ya Mwenyezi-Mungu huitikisa mivule,

hukwanyua majani ya miti msituni,

na hekaluni mwake wote wasema:

“Utukufu kwa Mungu!”

10 Mwenyezi-Mungu ameketi juu ya gharika;

Mwenyezi-Mungu ni mfalme atawalaye milele.

11 Mwenyezi-Mungu na awape watu wake nguvu!

Mwenyezi-Mungu na awabariki watu wake kwa amani!