Zaburi 20

Kuomba ushindi

(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Daudi)

1 Mwenyezi-Mungu akujibu uwapo taabuni;

jina la Mungu wa Yakobo likulinde.

2 Akupelekee msaada kutoka hekaluni mwake;

akutegemeze kutoka mlima Siyoni.

3 Azikumbuke sadaka zako zote;

azikubali tambiko zako za kuteketezwa.

4 Akujalie unayotamani moyoni mwako,

aifanikishe mipango yako yote.

5 Tutashangilia kwa ajili ya ushindi wako;

tutatweka bendera kulitukuza jina la Mungu wetu.

Mwenyezi-Mungu akutimizie maombi yako yote!

6 Najua Mwenyezi-Mungu atamsaidia mfalme aliyemteua,

atamjibu kutoka patakatifu pake mbinguni;

kwa mkono wake wa kulia atamjalia ushindi mkubwa.

7 Wengine hujigamba kwa magari ya vita;

wengine hujigamba kwa farasi wao.

Lakini sisi twajivunia Mwenyezi-Mungu, Mungu wetu.

8 Hao watajikwaa na kuanguka;

lakini sisi tutainuka na kusimama imara.

9 Umjalie mfalme ushindi, ee Mwenyezi-Mungu;

utujibu wakati tunapokuomba.