Zaburi 14

Uovu wa watu

(Kwa Mwimbishaji. Zaburi ya Daudi)

1 Wapumbavu hujisemea moyoni:

“Hakuna Mungu.”

Wote wamepotoka kabisa,

wametenda mambo ya kuchukiza;

hakuna hata mmoja atendaye jema!

2 Mwenyezi-Mungu anawaangalia wanadamu kutoka mbinguni,

aone kama kuna yeyote mwenye busara,

kama kuna yeyote anayemtafuta Mungu.

3 Lakini wote wamekosa,

wote wamepotoka pamoja;

hakuna atendaye mema,

hakuna hata mmoja.

4 “Je, hao watendao maovu hawana akili?

Wanawatafuna watu wangu kama mikate;

wala hawanijali mimi Mwenyezi-Mungu.”

5 Hapo watashikwa na hofu kubwa,

maana Mungu yu pamoja na waadilifu.

6 Unaweza kuvuruga mipango ya maskini,

lakini Mwenyezi-Mungu ndiye kimbilio lake.

7 Laiti ukombozi wa Israeli ungefika kutoka Siyoni!

Mwenyezi-Mungu atakaporekebisha hali ya watu wake,

wazawa wa Yakobo watashangilia;

Waisraeli watafurahi.