Zaburi 10

Sala dhidi ya udhalimu

1 Ee Mwenyezi-Mungu, mbona wasimama mbali?

Kwa nini wajificha wakati tumo taabuni?

2 Kwa kiburi waovu wanawatesa maskini;

njama zao ziwanase wao wenyewe.

3 Mwovu hujisifia tamaa zake mbaya,

mtu wa tamaa hulaani na kumkataa Mwenyezi-Mungu.

4 Katika majivuno yake husema: “Mungu hatagundua.”

Mawazo yake yote ni: “Hakuna Mungu.”

5 Njia za mwovu hufanikiwa daima;

kwake hukumu zako ziko mbali na mawazo yake,

na huwadharau maadui zake wote.

6 Huwaza moyoni: “Sitakuwa na wasiwasi;

sitapatwa na dhiki maishani.”

7 Kinywa chake kimejaa laana, udanganyifu na dhuluma;

mwepesi kusema maneno ya kuchukiza na maovu.

8 Hujificha vijijini huku anaotea,

amuue kwa siri mtu asiye na hatia.

Yuko macho kumvizia mnyonge;

9 huotea mafichoni mwake kama simba.

Huvizia apate kuwakamata maskini;

huwanasa kwa mtego wake na kuwachukua.

10 Mnyonge huvamiwa na kuangushwa chini;

huangushwa kwa ukatili wa mtu mwovu.

11 Mwovu huwaza moyoni mwake: “Mungu amesahau;

ameficha uso wake, haoni kitu!”

12 Inuka, ee Mwenyezi-Mungu, uwaadhibu;

usiwasahau wanaodhulumiwa.

13 Ee Mungu, kwa nini mwovu anakudharau,

na kusema ati hutamfanya awajibike?

14 Lakini wewe wawaona wenye dhiki na shida;

nawe daima uko tayari kuwasaidia.

Mnyonge anakutegemea wewe, ee Mungu,

wewe umekuwa daima msaada wa yatima.

15 Uzivunje nguvu za mtu mwovu;

ukomeshe uovu wake wote, usiwepo tena.

16 Mwenyezi-Mungu ni mfalme milele na milele!

Mataifa yasiyomjua yatatoweka nchini mwake.

17 Ee Mwenyezi-Mungu, wapokea dua za mnyonge;

wampa moyo na kumtegea sikio.

18 Utawatendea haki yatima na wanaodhulumiwa,

binadamu aliye udongo asiweze tena kuleta hofu.