Zaburi 8

Utukufu wa Mungu na cheo cha binadamu

(Kwa Mwimbishaji: Mtindo wa Gitithi. Zaburi ya Daudi)

1 Ee Mwenyezi-Mungu, Bwana wetu,

kweli jina lako latukuka duniani kote!

Utukufu wako waenea mpaka juu ya mbingu!

2 Kwa sifa za watoto wadogo na wanyonyao,

umejiwekea ngome dhidi ya adui zako,

uwakomeshe waasi na wapinzani wako.

3 Nikiangalia mbingu, kazi ya vidole vyako,

mwezi na nyota ulizozisimika huko,

4 mtu ni nini, ee Mungu, hata umfikirie,

binadamu ni nini hata umjali?

5 Umemfanya awe karibu kama Mungu,

umemvika fahari na heshima.

6 Ulimpa madaraka juu ya kazi zako zote;

uliviweka viumbe vyote chini ya mamlaka yake:

7 Kondoo, ng’ombe, na wanyama wa porini;

8 ndege, samaki, na viumbe vyote vya baharini.

9 Ee Mwenyezi-Mungu, Bwana wetu,

kweli jina lako latukuka duniani kote!