Zaburi 6

Sala wakati wa taabu

(Kwa Mwimbishaji: Na ala za nyuzi za muziki. Mtindo wa Sheminithi. Zaburi ya Daudi)

1 Ee Mwenyezi-Mungu, usinikemee kwa hasira yako;

usiniadhibu kwa ghadhabu yako.

2 Unihurumie, ee Mwenyezi-Mungu, nimeishiwa nguvu;

uniponye, ee Mwenyezi-Mungu, nataabika mpaka mifupani.

3 Ninahangaika sana rohoni mwangu.

Ee Mwenyezi-Mungu, utakawia mpaka lini?

4 Unigeukie, ee Mwenyezi-Mungu, uniokoe;

unisalimishe kwa sababu ya fadhili zako.

5 Huko kwa wafu hakuna anayekukumbuka;

huko kuzimu ni nani awezaye kukusifu?

6 Niko hoi kwa kilio cha uchungu;

kila usiku nalowesha kitanda changu kwa machozi;

kwa kulia kwangu naulowesha mto wangu.

7 Macho yangu yamechoka kwa huzuni;

yamefifia kwa kutaabishwa na adui.

8 Ondokeni kwangu enyi nyote watenda maovu!

Maana Mwenyezi-Mungu amesikia kilio changu.

9 Mwenyezi-Mungu amesikia ombi langu;

Mwenyezi-Mungu amekubali sala yangu.

10 Maadui zangu wote wataaibika na kufadhaika;

watarudi nyuma na kuaibishwa ghafla.