Zaburi 4

Kuomba msaada jioni

(Kwa Mwimbishaji: Na ala za nyuzi za muziki. Zaburi ya Daudi)

1 Ee Mungu mtetezi wa haki yangu, unijibu niombapo.

Nilipokuwa katika shida, wewe ulinisaidia;

unionee huruma na kusikia sala yangu.

2 Jamani, mtaniharibia jina langu mpaka lini?

Mpaka lini mtapenda upuuzi na kusema uongo?

3 Jueni kuwa Mwenyezi-Mungu amejiteulia mwaminifu wake.

Mwenyezi-Mungu husikia kila ninapomwomba.

4 Tetemekeni kwa hofu na msitende dhambi;

tafakarini vitandani mwenu na kunyamaza.

5 Toeni tambiko zilizo sawa,

na kumtumainia Mwenyezi-Mungu.

6 Wengi husema: “Laiti tungepata tena fanaka!

Utuangalie kwa wema, ee Mwenyezi-Mungu!”

7 Lakini mimi umenijalia furaha kubwa moyoni,

kuliko ya hao walio na divai na ngano kwa wingi.

8 Nalala na kupata usingizi kwa amani;

ee Mwenyezi-Mungu, wewe peke yako waniweka salama.