Zaburi 3

Kuomba msaada asubuhi

(Zaburi ya Daudi alipomkimbia Absalomu)

1 Ee Mwenyezi-Mungu, tazama walivyo wengi adui zangu,

ni wengi mno hao wanaonishambulia.

2 Wengi wanasema juu yangu,

“Hatapata msaada kwa Mungu.”

3 Lakini wewe ee Mwenyezi-Mungu u ngao yangu kila upande;

kwako napata fahari na ushindi wangu.

4 Nakulilia kwa sauti, ee Mungu,

nawe wanisikiliza kutoka mlima wako mtakatifu.

5 Nalala na kupata usingizi,

naamka tena maana wewe ee Mwenyezi-Mungu wanitegemeza.

6 Sitayaogopa maelfu ya watu,

wanaonizingira kila upande.

7 Uje ee Mwenyezi-Mungu!

Niokoe ee Mungu wangu!

Wewe wawavunja mataya maadui zangu wote;

wawavunja meno waovu wasinidhuru.

8 Mwenyezi-Mungu ndiwe uokoaye;

uwape baraka watu wako.