Yobu 16

Jibu la Yobu

1 Hapo Yobu akajibu:

2 “Mambo kama hayo nimeyasikia mengi;

nyinyi ni wafariji duni kabisa!

3 Mwisho wa maneno haya matupu ni lini?

Au ni kitu gani kinachowachochea kujibu?

4 Kama nyinyi mngekuwa mimi, na mimi nyinyi,

ningeweza kusema kama nyinyi

ningeweza kubuni maneno dhidi yenu,

na kutikisa kichwa changu.

5 Ningeweza kuwatia moyo kwa maneno yangu,

na maneno yangu ya faraja yangewatuliza.

6 “Lakini nikisema maumivu yangu hayatulii,

na nikikaa kimya hayaondoki.

7 Kweli Mungu amenichakaza

ameharibu kila kitu karibu nami.

8 Amenifanya ninyauke, na huo ni ushindi dhidi yangu.

Kukonda kwangu kumenikabili

na kushuhudia dhidi yangu.

9 Amenirarua kwa hasira na kunichukia;

amenisagia meno;

na adui yangu ananikodolea macho.

10 Watu wananidhihaki na kunicheka;

makundi kwa makundi hunizunguka,

na kunipiga makofi mashavuni.

11 Mungu amenitia mikononi mwa wajeuri,

na kunitupa mikononi mwa waovu.

12 Nilikuwa nimestarehe, lakini akanivunjavunja,

alinikaba shingo na kunipasua vipandevipande;

alinifanya shabaha ya mishale yake,

13 akanipiga mishale kutoka kila upande.

Amenipasua figo bila huruma,

na nyongo yangu akaimwaga chini.

14 Hunivunja na kunipiga tena na tena;

hunishambulia kama askari.

15 “Nimejishonea mavazi ya gunia,

fahari yangu nimeibwaga mavumbini.

16 Uso wangu ni mwekundu kwa kulia,

kope zangu zimekuwa nyeusi ti;

17 ingawa sijafanya dhuluma kwa mkono wangu,

na sala zangu kwa Mungu ni safi.

18 “Ewe dunia, usiifunike damu yangu iliyomwagika;

kilio changu kienee kila mahali.

19 Nina hakika ninaye shahidi wangu mbinguni,

mwenye kunitetea yuko huko juu.

20 Rafiki zangu wanidharau;

nabubujika machozi kumwomba Mungu.

21 Laiti mtu angenitetea mbele ya Mungu,

kama ifanyikavyo duniani kati za watu wawili.

22 Naam, miaka yangu ni michache,

nami nitakwenda huko ambako sitarudi.