Zekaria 13

1 “Siku hiyo, kutatokea chemchemi ya kuwatakasa dhambi na unajisi wazawa wa Daudi na wakazi wote wa Yerusalemu.

2 Wakati huo, nasema mimi Mwenyezi-Mungu wa majeshi, majina ya vinyago vya miungu nchini nitayaondoa, wala hayatakumbukwa tena. Na wanaojidai kuwa manabii nitawaondolea mbali pamoja na tamaa zao za kuabudu sanamu.

3 Mtu yeyote akijidai kuwa nabii, baba na mama yake waliomzaa watamwambia, ‘Unapaswa kufa kwa kuwa unasema uongo kwa jina la Mwenyezi-Mungu’. Na haohao wazazi wake watamchoma kisu akiwa anatabiri.

4 Siku hiyo, kila nabii atayaonea aibu maono yake anapotabiri. Hawatavaa mavazi ya manyoya ili kudanganya watu,

5 bali kila mmoja atasema, ‘Mimi si nabii. Mimi ni mkulima tu; nimeimiliki ardhi tangu ujana wangu’.

6 Na mtu akimwuliza mmoja wao, ‘Vidonda hivi ulivyo navyo mgongoni vimetoka wapi?’ Yeye atajibu, ‘Vidonda hivi nilivipata katika nyumba ya rafiki zangu.’”

7 Mwenyezi-Mungu wa majeshi asema hivi:

“Amka, ee upanga!

Inuka umshambulie mchungaji wangu;

naam, mchungaji anayenitumikia.

Mpige mchungaji na kondoo watawanyike.

Nitaunyosha mkono wangu,

kuwashambulia watu wadhaifu.

8 Theluthi mbili za watu katika nchi zitaangamizwa;

ni theluthi moja tu itakayosalimika.

9 Theluthi hiyo moja itakayosalia,

nitaijaribu na kuitakasa,

kama mtu asafishavyo fedha,

naam, kama ijaribiwavyo dhahabu.

Hapo wao wataniomba mimi,

nami nitawajibu.

Nitasema, ‘Hawa ni watu wangu’,

nao watasema, ‘Mwenyezi-Mungu, ndiye Mungu wetu.’”